MALAIKA MWEUSI EPISODE 7

Emmanuel Lee
By -
0



HADITHI: MALAIKA MWEUSI

EPISODE 7

MTUNZI: Ally Mbetu ‘DrAmbe’

SIMU: 0713 646500

ILIPOISHIA:EPISODE 6


Ikawa asubuhi naingia kutafuta kuni na kushughulikia kilimo kilichoachwa na babu.  Nilijikuta namaliza miezi mitatu bila kutegemea. Siku moja niliporudi shamba nilikuta mwili wa mtu aliyekufa. Nilikimbia mbio hadi nyumbani babu alishangaa na kuniuliza kulikoni nilimuelezea nilivyoona.

SASA ENDELEA...


     “Basi mjukuu wangu hayo ya kawaida la muhimu uufukie ule mwili .“

     “Hapana babu wanaweza kuniua.”

     “Kama kufa ningekufa mimi huu ni mwaka wa nne nipo huku na nishazika watu si chini ya mia mbili rudi ukazike mjukuu wangu.”

    “ Hapana babu sirudi,” nilikataa.

    “Usiogope kumbuka usipouzika utajiletea matatizo.“

    “Matatizo! Matatizo gani?”

    “Ule mwili ukioza patakuwa hapakaliki harufu ya mwanadamu ni kali sana.“

Nilijipa moyo nikarudi kuuzika mwili wa yule mtu alikuwa msichana, nilishangaa alikuwa amevaa hereni na mkufu wa bei mbaya nilijiuliza ina maana waliomuua shida yao ilikuwa ni nini? Nilichimba na kuufukia ule mwili .

   Tangu hapo nikaanza kuwa na moyo wa ujasiri nilishangaa woga ulinitoka hata nilipokuta mwili mwingine niliufukia bila hofu yoyote. Siku moja nilirudi kutoka kwenye kilimo chetu, tena siku hiyo nilikuwa nimekamata kware nilijua babu Utakufalini atafurahia na kuona nimeanza kumrithi katika uwindaji.

 Nilimkuta Kalekwa analia babu alikuwa amelala tu, si kawaida yake kumuacha Kalekwa alie kiasi kile. Nilipofika nilimnyanyua na kumbembeleza, baada ya kunyamaza nilimfuata babu Utakufalin. Nilishangaa kumkuta amelala wakati mjukuu wake alikuwa analia. Nilimuamsha alifumbua macho lakini macho yake yalikuwa mazito. 

“Babu vipi?”

“Ha…a…a…a….apa..na,” aliongea kwa shida .

“Babu nimerudi, tena leo nimekuletea kitoweo.“

 “Thereza,“ babu aliniita kwa sauti ya chini.

 “Abee babu,” niliitaka huku nilimuinamia ili nimsikilize vizuri.

 “Mtu …nze..Ka..le..kwa.”

 “Ba..bu..vipi?”

 Babu alinyoosha mkono aliokuwa ameukunja ngumi na kunipa kitu nilipokea hakikuwa kingine  zaidi ya kile alichonionyesha na matumizi yake. Nilipokipokea tu  swali la jina jina lake kuwa atakufa lini ilitimia, baada ya kupokea kile kizizi babu alikata roho.

  Nilishindwa kulia japo roho iliniuma ,yaani dhamira yangu ya kulipa fadhila iliyeyuka kama donge la mafuta kwenye kikaango cha moto. Nilitamani kulia lakini nilijikaza, najua udhaifu ninapolia hasa msiba uwe unanihusu. Kwa kiasi gani babu Utakufalini alivyookoa maisha yangu nilijua kilio changu cha kawaida lazima nitapoteza fahamu kitu kitakachomfanya Kalekwa apate shida.

Nilijikaza kiume na kuchimba kaburi kisha niliuzika mwili wa shujaa wangu mzee Jacob au maarufu kama Utakufalini mtu aliyekufa kifo kama mnyama kutokana na roho mbaya za watu wanaoonekana nje kondoo lakini ndani ni wanyama wakali kushinda mbwa mwitu. 

Niliuzika mwili wa mtu muhimu maishani mwangu, roho iliniuma lakini ndio hivyo Mungu amemuita. Mimi nilimpenda lakini yeye alimpenda zaidi. Baada ya mazishi siku ya pili alfajiri nilianza safari kurudi mjini njia ya pori na pori kutafuta barabara. Ungeniangalia ungesema labda ni mzuka jinsi nilivyokuwa na Kalekwa, tulikuwa na nywele ndefu utafikiri mizimu iliyofufuka, miili yetu ilikuwa imepauka na vumbi jingi. Nguo zetu chafu na zilizochanika zilituweka nusu uchi, nilianza safari ambayo kidogo ilikuwa ngumu. 

Nilimbeba Kalekwa mgongoni kuanza safari nisiyojua naelekea wapi. Pori lilikuwa linatisha niliweza kupishana na wanyama wakali kama Simba, Chui, Tembo hata Vifaru. Kizizi nilichopewa na babu ndicho kilichonisaidia kusafiri salama, nilisafiri saa kumi na mbili nilipumzika na mdogo wangu Kalekwa kupata chakula na kujilaza hadi siku ya pili.

Siku iliyofuata alfajiri niliianza safari yangu, nilitembea kwa muda wa siku tatu hadi kukutana na barabara kuu ya magari. Tulipokuwa tunakaribia barabarani nilisikia watu wakiongea. 

" Eeeh bwana jisaidie haraka tunataka Dar tufike saa nne usiku."

 Nilibadili njia na kutokea upande mwingine lakini si mbali nao, mbele nilikuta lori la mizigo. Nilimshukuru Mungu kimoyomoyo nilitaka kuwaomba lakini hali yetu kama mizimu iliyofufuka nani angetukubalia au wangetaka kutuhoji na kutufikisha polisi niliona  mambo yanaweza kuwa kama ya mzee Utakufalini afanyiwe ukatili ategemee polisi wamsaidie ndio kwanza wanamkandamiza na kumbambikia kesi nzito ya mauaji.

 Niliamua kutumia ukomandoo wangu kama ndani ya sinema, nilinyata taratibu na kuwazunguka na kwenda kupanda nyuma kwenye mizigo. Muda si mrefu safari ilianza. Nilimuomba Mungu anifikishe salama. Dua yangu ilisikiliozwa tulisafiri bila tatizo  gari liliingia Dar saa 4.30 usiku. 

Kama kawaida yangu niliruka kwenye gari lilipokuwa limesimama taa za barabarani za maeneo ya Ubungo. Nilianza safari ya kuelekea kwangu, nilifika kwangu majira ya saa kumi alfajiri. Niligonga geti mlinzi alihoji kabla ya kufungua, nilimweleza ni mimi. Alipofungua alishangaa hali niliyokuwa nayo kwanza alinikatalia katakata kuwa si mimi. Baada ya kumuelewesha  aliniruhusu kuingia ndani.

 Alitaka kujua nini kilichomsibu hadi kuwa kwenye hali ile nilimweleza aniache nipumzike kwanza. Niliingia hadi ndani cha kwanza niliyesimama mbele ya kioo nilikuwa sina tofauti na mabush man. Kabla ya yote nilijipiga picha mimi na Kalekwa ili niweke kumbukumbu kwenye maisha yangu.

Nimekubali maneno ya babu Utakufalini kuwa tembea uone na kuishi kwingi kuona mengi. Baada ya kupiga picha kadhaa za ukumbusho ambazo ni hizi,” Malaika Mweusi alivuta droo na kutoa bahasha ambayo alimpa Anderson ambaye alizitazama na jinsi walivyokuwa kama wanyama.

 Baada ya kuzitazama kwa muda alimrudishia bila kusema neno, Malaika Mweusi akaendelea:

“ Basi niliingia bafuni kuoga na kumwosha Kalekwa kisha tulijitupa kitandani na usingizi mzigo ulitupitia. Kutokana na uchovu niliamka siku ya pili saa kumi jioni kwa msaada wa Kalekwa aliyehi kuamka. Niliamka mwili ukiwa umechoka na njaa ilikuwa unauma kama kidonda, nilipiga simu Shoprite watuletee chakula.

 Vilevile niligundua akili ya Kalekwa ilikuwa ya kiporipori kama angeendelea kuishi porini  angekuwa kama mnyama. Kila kitu kilikuwa kigeni wakati huo alikuwa na miaka miwili. Umri wa Kalekwa ulinijulisha  kumbe nilikaa kule porini kwa miaka miwili.

Baada ya kujirudisha hali ya ubinadamu, Sikutaka kupoteza muda lilikwenda moja kwa moja kwa Doctor Ray. Aliponiona hakuamini alinikumbatia kwa furaha. Hakuficha furaha yake na kuniuliza.

"Ulipotelea wapi Mr embo afadhali umeonekana kuna kazi inawaumiza akili watu, nina imani ufumbuzi ni wewe kama utaifanya vizuri malipo yake nina imani ni makubwa si chini ya bilioni moja."

"Kazi gani hiyo yenye pesa nyingi hivyo?”

Habari hizi zilinishtua ni kazi gani tena hivyo yenye malipo mazito pesa ambazo sikuwaza kuzipata maishani bilioni mia moja, mmh hapana ni kazi gani hii ambayo imesababisha moyo upasuke kwa mshtuko.

"Ray ni kazi gani hiyo yenye malipo kama hayo ambayo naona kama ndoto, au umekosea kusema?" nilishtuka.

"Hapana Thereza malipo ya kazi ni bilioni 100 kama utakubali advance shilingi bilioni 60 pale utakapo kuwa tayari kuifanya."

"Mmh! Mbona unanitisha ni kazi gani?"

"Utaelewa tu, vipi ulisafiri?"

“We acha niliyonikuta Mungu anajua nahitaji msaada wako mwingine,” nilimwambia Dokta Ray.

"Unashinda gani? Sema tu nipo tayari kukusaidia kwa hali na mali."

"Twende ofisini kwako," niliongozana na Dokta Ray japo yeye anapenda nimwite Mr Ray hadi ofisini mwake.

Nikiwa ofisini mwake aliniletea glasi iliyo jaa whisky ilikuwa  miaka miwili imepita bila kutumia kilevi chochote. Sikuwa na haja tena ya kuendelea kunywa pombe kali.

Nilijua ule ndio wakati muafaka wa kuacha pombe kali ikiwezekana kuacha kabisa unywaji wa pombe. Nilimtaka radhi Mr Ray.

"Samahani Mr Ray situmii pombe." 

 "Hata bia?"

"Pombe ya aina yoyote."

“Ooh! Sasa itakuwaje na kwenye friji yangu kuna maji tu."

"Maji yanatosha sana," alinijazia maji kwenye glasi baada ya kukaa na kuitengeneza sauti yake alisema:

"Ehe...Thereza kwanza habari za siku?"

"Mbaya."

"Mbaya! Una maana gani?"

"Ndio maana nimerudi tena kwako.”

“Nina imani unakumbuka vizuri sababu iliyonileta hapa mara ya kwanza?"

"Ndio nakumbuka vizuri, kama sikosei ni tukio la kubakwa."

"Sawasawa kabisa."

"Vipi umebakwa tena?"

"Bora ningebakwa nikajua moja.”

“Sasa umepata masahibu gani?”

 Nilianza kumwelezea kisa chote kilichonitokea mwanzo hadi siku ile nipokuwa  mbele yake kama golikipa aliye okoa penati za Ziraili.

Habari zile zilinisisimua Dl Ray mpaka rangi yake nyeupe kuwa nyekundu. Aliniangalia mara mbili mbili kisha alishusha pumzi na kusema:

“Pole sana Thereza, wewe ni mwanamkae wa shoka, nina imani kwa hatua zote ulizopitia hautasita kuifanya kazi yetu.”

"Dk Ray niweke wazi ni kazi gani? Mbona moyo wangu unalipuka."

"Kwanza kabla sijakueleza ni kazi gani la muhimu  kuishughulikia afya yako."

Niliongozana na Dk Ray hadi chumba cha uchunguzi na kuyachunguza makovu yangu sehemu za siri yaliyoniweka kwenye shepu mbaya.

Baada ya uchunguzi tulirudi ofisini kwake, aliniacha kidogo na kuingia kwenye chumba kimoja. Baada ya dakika kama tano alirudi na bahasha kubwa kidogo pamoja na kitabu kikubwa na kuviweka mezani.

Alinieleza nizunguke upande wake, baada ya kufanya hivyo alinifungulia kile kitabu kilichokuwa na picha za watu wenye majeraha na makovu ya kutisha na picha zingine wale watu wakiwa wamepona.

Kisha alinitolea picha za kawaida na kunionyesha watu waliopata matibabu kwenye hospitali yake walioungua moto lakini baada ya matibabu ya ngozi zao hurudi kwenye hali ya kawaida.

Vilevile watu wenye makovu ya kutisha waliofanyiwa upasuaji pale na hali zao zilivyo kuwa nzuri, huwezi kuamini kama hapo awali alikuwa na jeraha au kovu.

"Sasa Ther eza kazi yako ni ndogo nitaifanya kwa wiki tatu utakuwa mzima kabisa, kwa maelezo yako yule mzee aliyeokoa maisha yako dawa zake zilifanya kazi kubwa bila hivyo lazima ungekufa au kuoza kizazi mpaka utumbo kazi yangu ni upasuaji mdogo kuna dawa za kuponyesha kidonda kwa wiki kunakuwa kumepona vilevile kuna dawa za sindano zinazo kausha kidonda kabla ya kupakwa dawa juu ya kidonda ambayo hugeuka ngozi, ninajua utashangaa  jinsi utakavyopona."

"Nitashukuru sana, sijui gharama zake ni shilingi ngapi?”

"Hapana sihitaji pesa yako zaidi ya kunikubalia kuifanya hiyo kazi."

"Usiwe na wasiwasi sitakuangusha kwa vile wewe ni mtu muhimu sana kwangu nina imani nitaifanya hiyo kazi bila pingamizi," nilijikuta nakubali bila kujua ni kazi gani.

"Waawoo Thereza katika siku uliyonifurahisha ni leo na mimi nakuahidi kukupa ushirikiano wa kutosha," Dk Ray alifurahi sana bila kujua sababu ya furaha yake na kazi anayotaka kunipa.

"Nitashukuru."

"Sasa sijui matibabu tutaanza lini?"

"Nilipendelea hata leo lakini kwa vile nina mdogo wangu ambaye hajuani na mtu yeyote lazima nimtengenezee mazingira mazuri kesho kutwa nitarudi kwa ajili ya matibabu.

Niliamua kuagana na Dk Ray ili nizungukie miradi yangu kujua maendeleo yake baada ya kutoweka kwa miaka miwili na ushee si mchezo unaweza kukuta mabadiliko makubwa.

Kabla ya kuagana Dk Ray alinieleza nisubiri kidogo alinyanyua simu moja, machoni kwangu ndio mara yangu ya kwanza kuiona. Ipo kama radio call, lakini ni ndogo sawa na simu za kawaida.

"Haloo mkuu yule mtu ameonekana.”

“Nani huyo?” kwa vile ilikuwa sauti inayosikika nilisikia maongezi yao.

“Thereza."

“Thereza ndio nani?"

"Yule msichana wa kazi ya PT."

"Ooh. samahani si unajua mambo mengi vipi amekubali?”

"Ndio amekubali.”

"Vizuri sana yupo tayari kuianza kazi?"

"Ndio nimekutana naye, vilevile ana matatizo anahitaji msaada wetu japo yeye mwenyewe yupo tayari kujilipia."

"Vizuri, anatatizo gani?" 

Dk  Ray alimweleza mtu wa upande wa pili tatizo langu.

“Ooh, siyo tatizo hakikisha anapata matibabu ya hali ya juu ya yatayomponyesha vizuri,  nina imani unaelewa umuhimu wake?”

"Ndiyo bosi."

“Sasa, kwanza hata sijui niseme nini yaani kupatikana kwa binti huyo kumenipa matuini ya ajabu najishangaa hata furaha imemjaa ghafla nina imani binti ataifanikisha vizuri na mhakikishia akiifanya vizuri nitamuongezea bilioni 30 kama asante, matibabu anaanza lini?"

"Kesho kutwa bosi."

"Vizuri mpe shilingi 150 ili zimsaidie kipindi cha matibabu yake."

“Sawa bosi."

“Hakikisha vitu muhimu vinakuwa tayari ili amalizapo matibabu aanze kazi mara moja.''

“Hamna tatizo bosi."

“Ok bai kazi njema."

Baada ya maongezi Dk Ray alishusha pumzi nzito kisha alisema:

"Thereza subiri," aliingia tena kwenye kile chumba na kurudi na mfuko mkononi aliuweka juu ya meza na kuufungua.

Ulikuwa na maburungutu ya pesa zilizokuwa zimefungwa mafungu matano.

"Hizi ni milioni 150 unaweza kuzihesabu."

"Za nini zote hizi?"

“Nina imani miaka miwili uliyoipoteza umepoteza na kipato chako hivyo  zitakusaidia wakati wa matibabu."

"Sawa, lakini ni nyingi sana wakati kazi yenyewe bado sijaifanya," pesa zile zilinitisha.”

"Sawa, wacha nikapumzike ili nihakikishe namtengenezea mdogo wangu mazingira mazuri kipindi chote nikiwa katika matibabu yangu," nilisema huku nikizirudisha zile pesa kwenye mfuko ili niondoke zangu.

“Zihesabu ili uzihakikishe.”

“Sina wasi wasi nawe nakuamini," niliubeba mzigo wangu na kuagana na Dk Ray.

Nikiwa narudi Dar nilijawa na mawazo mengi juu ya kazi nitayopewa, nilijiuliza ni kazi gani hiyo ambayo wanamwaga mamilion hata bila wasiwasi wowote.

Niliamua kuachana na mawazo juu ya kazi hiyo kwani kuwaza sana niliona  ni kuiumiza akili yangu kwa kitu nisicho kijua.

 Niliamua kuachana na kazi ya kuiwaza kazi hiyo ili kusubiri mpaka hapo nitapo elezwa ni kazi gani. Lakini ajabu kila nilipoiwaza kazi hiyo moyo  ulinilipuka na kujawa na hofu moyoni. Lilibakia swali kichwani juu ya kazi ninayotaka kupewa.

Malipo billioni 100 advance bilioni 60 pesa za matumizi nje ya malipo milioni150.

Kwa upande mwingine nilijilaumu kukubali  bila kuijua, nilijiuliza kama nikiikataa je itakuwaje. Wasiwasi wangu ulikuwa katika kukosa matibabu ambayo yalikuwa muhimu kwangu kuliko kitu chochote.

Nilijiuliza kwa nini niendelee kuumiza akili yangu na kuisubiri kazi hiyo watakayonipa. Wakati huo nilikuwa naaingia kwenye geti la moja ya makampuni yangu.

Siku hiyo nilizungurukia miradi yangu yote , nilimshukuru Mungu kukuta maendeleo vizuri vilevile niliwatembelea washirika wenzangu niliokuwa nao wakati wa uchokoraa.

Nao waliendelea vizuri waliponiona walifurahi sana kuniona nami vilevile nilifurahi. Siyo siri kila ninapowaona washirika wenzangu nlikumbuka mengi kweli maisha yanabadilika.

Tabu za kushinda juani ndizo zinazo niumiza roho sikuwa tayari kuona ombaomba au watoto wanaozurura mitaani. Nazidi kumshukuru Mungu hali   ilikuwa inaridhisha japo ripoti ya mikoani ilinifanya niongeze vituo vingi vya watoto.

Nilipanga pesa nitayoipata kwa ajili ya kazi ambayo siijui robo ya pesa hizo ambazo ni bilioni 25 billioni 10 kuongeza vituo na shule pamoja na billioni 15 kujenga kiwanda kitachoongeza ajira kwa vijana.

Baada ya ziara yangu iliyoonyesha mafanikio makubwa pamoja na ongezeko la misaada ya wahisani iliyofikia dola millioni moja. Nilimkabidhisha Kalekwa kwa mlezi ambaye atamlea kipindi chote nitakuwa katika matibabu.

Matibabu yangu yalikwenda vizuri, ndani ya wiki tatu nilikuwa mzima wa afya njema kabisa sikuwa na kovu lolote mwilini kwangu. Kweli nimeamini dawa zipo.

Baada ya matibabu na mapumziko ya wiki mbili zingine, niliitwa ofisini kwa Dk Ray ambaye alinijulisha kuwa nijiandae safari ambayo ingekuwa baada ya wiki.

Ilikuwa kwa ajili ya mazoezi ya mwaka mzima kabla ya kuianza kazi ambayo ilihitaji mafunzo ya hali ya juu.

Nilikabidhiwa milioni 500 kwa ajili ya kuacha nyumbani  kama kuna mtu anamtegemea. Sio siri kila muda na dakika nilijiuliza ni kazi gani yenye mafunzo ya mwaka mzima.

Baada ya kurekebisha mambo yangu niliwasili Kibaha kwa ajili ya safari ya mwaka mzima nisiyo jua na kwenda wapi. Majira ya saa moja usiku nilipakiwa ndani ya gari aina ya Toyota Land Cruser V8 na safari ilianza. Ilikuwa safari ya kurudi Dar.

Lakini kabla ya kuingia Dar nilifungwa kitambaa usoni nilipouliza niliambiwa ni mwanzo wa mazoezi. Nilipandishwa ndege nikiwa nimefungwa kitambaa usoni. Ndani ya Ndege wakati ikiwa angani nilifunguliwa kitambaa usoni.

Ndani ya ndege kulikuwa na watu zaidi ya hamsini kila mmoja alikuwa kimya.

Tulisafiri kwa muda wa siku mbili. Siku ya pili ndege ilitua ilikuwa ni usiku wa manane, tuliteremka sikujua ule ni mji gani hata nilipo wauliza wenzangu nao walisema hawajui lakini ni moja ya nchi za Ulaya.


Hata nilipo muuliza mkuu wa msafara alinijibu eti nilichofuata ni mafunzo sio kujua ule ni mji gani au nchi gani.

Kesho yake asubuhi tuliamshwa na kukumbiza mchakamchaka, maisha yale hayakuwa mageni kwangu kwani hayana tofauti na yale niliyoishi na mzee Utakufalini ni ukomandoo tosha.

Tofauti yake mafunzo yalikuwa ya kisasa yenye kukufanya mwanadamu uwe na moyo wa chuma roho ya kinyama ya kumuua mwanadamu mwenzio kama unaua nzi. Nilijifunza vitu vingi kutumia silaha za kila aina, vifaa vyote vya electr onic kutumia vyombo vyote vya kisasa.

Niliweza kuongea lugha zaidi ya tano kiswahili kiingereza, kifaransa, kiarabu na kitaliano. Vilevile nilikuwa na uwezo wa kuigiza sauti tofauti zaidi ya ishirini.

Nilifuzu mbinu za mapigano ya silaha na mikono baada ya kuhitimu mafunzo nilirudi Tanzania kwa mtindo uleule nilioondokea wa kufungwa kitambaa usoni.

Baada ya kufika nyumbani Tanzania nilipewa mapumziko ya wiki mbili kabla ya kujulishwa ni kazi gani iliyo mbele yangu iliyoonekana nzito. Lakini kulikuwa na tofauti kati ya mwanzo na muda ule.

Mwanzo nilipokuwa nikiifikiria hiyo kazi nisiyoijua moyo uliingia hofu na woga mwingi ulinitawala. Lakini baada ya kurudi kutoka kwenye mafunzo ya hatari sikuwa  tena na woga hata chembe, nilikuwa tayari kwa kazi yoyote iliyo mbele yangu. 

Baada ya mapumziko niliitwa Kibaha tayari kukabidhiwa hiyo kazi, kama kawaida nilikutana na Dk Ray:

"Ooh karibu mrembo."

“Asante.”

“Nina imani upo tayari kwa kazi?”

“Ndio maana yake”

“Sawa, subiri wakubwa watafika muda si mrefu ili kukueleza cha kufanya

“Hakuna tabu.”

Nilikaribishwa sebuleni na kupewa kinywaji nikiwa nawasubiri hao wakubwa.

Niliendelea kupata kinywaji laini na kusoma magazeti ya siku ile.

 Mara kundi la watu wasiopungua kumi na mbili walinipita kuelekea chumba cha mikutano hakuna aliyenisalimia zaidi ya kupita kimyakimya. Nami sikuwasalimia nilitulia tuli nikisoma magazeti, mara alikuja Dk Ray na kunieleza:

“Thereza jiandae wazee wameisha kuja.”

“Nijiandae kwa kipi?” nilimuuliza.

“Ili kukabiliana na maswali yao.”

“Wana swali gani jipya ambalo halijawahi kuulizwa duniani?”

“Unaonekana unajiamini sana?” Dk Ray.

“Lazima nijiamini, ndio maana nipo hapa tayari kwa lolote.”

“Nilikuwa nakutaarifu tu.”

“Shaka ondoa nipo tayari kukabiliana na mtu yeyote kama niliweza kukabiliana na kifo, mwanadamu ni nini kwangu?”

“Mmh, sikuwezi.”

Dk Ray aliondoka na kuniacha nikisoma gazeti lakini mawazo yakiwa juu ya kikao hicho. Nilijikuta najiuliza swali la awali inaweza kuwa ni kazi gani. Hao wakubwa sio siri ni wakubwa kweli wengine wapo serikalini tena wana vyeo vya juu. wengie wapo taasisi za dini walio mbele katika kutoa misaada kwa jamii lakini wengine walikuwa  wageni machoni mwangu.

Kikao kilifanyika kwa zaidi ya saa mbili na mimi niliendelea kusubiri  mpaka nilipo fuatwa na Dk Ray.

“Vipi upo tayari?”

“Tayari kivipi?” nilimuuliza.

“Kuonana na wazee.”

“Nilikuwa tayari tangu nilipotoka nyumbani kwangu.”

“Basi tuongozane kwenye kikao ambacho nakiona ni kizito tofauti na vikao vyote.”

Niliongozana na Dk Ray hadi kwenye ukumbi wa mikutano uliokuwa mzuri uliojengwa kisasa.

Nilipoingia nilionyeshwa kiti kwa ishara ya mkono, kilikuwa kiti cha kati yaani kinachotazamana na mwenyekiti wa kikao. Baada ya kuketi  Ray alitoka nje ya chumba cha mikutano ikimaanisha kicheo ni mtu mdogo sana.

Baada ya kuketi alikuja msichana aliyevaa mavazi yaliyouacha uchi mwili wake kwa asilimia themanini. Kile kilinishtua yaani mhudumu ni tofauti kubwa na picha iliyokuwa ndani kwenye kikao cha watu wasio pungua kumi na mbili wenye heshima zao.

Walikuwepo  viongozi wa dini mbili viongozi wa serikali na viongozi wa mashirika ya dini ya nje na taasisi zisizo za kiserikali (NGO!S) za kitaifa na kimataifa. Nilijiuliza iweje  msichana alijiweka sehemu kubwa ya mwili wake uchi ndiye awe mhudumu wao?

Hapo kengele ya tahadhari ililia kichwani mwangu, niliachana na hilo kwa vile sicho nilichokifuata. Muhimu kwa muda ule kujua ni kazi gani ninayotaka kupewa.

Mhudumu aliyekuwa amesimama pembeni yangu aliniuliza:

“Dada unatumia kinywaji gani?” 

Wakati huo kila mmoja aliyekuwa mule ndani alikuwa akitumia pombe kali.

“Nipatie soda ya aina yeyote.”

“Ooh! Samahami dada yangu hakuna soda ya aina yeyote zaidi ya pombe kali na pombe zingine.”

“Maji yapo?”

“Ndio yapo.”

“Niletee.”

Mhudumu aliondoka baada ya muda alirudi na chupa kubwa ya maji pamoja na glasi. Baada ya kunijazia maji kwenye glasi aliondoka, wakati wote huo kikao kilikuwa kimya wakipitia nyaraka muhimu kila mmoja alikuwa ameinama akisoma. Wakiwa wanaendelea kupeuzi na mimi muda ule niliutumia kuwasoma sura zao.

Kati ya watu kumi na mbili sura sita nilizifahamu hazikuwa ngeni machoni mwangu ila sita kila nilivyojitahidi kuzikumbuka jibu lilikuwa mbali. Nilitulia tuli huku nikiendelea kuisoma mandhari ya mule ndani.

Nilishtuliwa na mlio wa meza iliyogongwa ikimaanisha tuwe tayari kumsikiliza mwenyekiti wa kikao ambaye hakuwa mwingine ila Father Gin mkuu wa kanisa la Watu waliojitolea kwa ajili ya Bwana.

Alikuwa ni mtu ninayemuheshimu sana ambaye ndiye kinara wa kutoa misaada si kwa wananchi tu hata serikali nayo iliuthamini mchango wake kwa maendeleo ya nchi.

“Karibu Thereza ilikuwa sauti yake nzito Father Gin.”

“Asante.”

“Kabla ya yote sister Caroline mwapishane ili awe tayari kwa kikao chetu.”

 Mmoja wa wajumbe wa mkutano alinyanyuka na kuja karibu yangu. Niliapishwa kiapo tofauti na viapo nilivyokwisha wahi kuona mtu akiapa. Kilikuwa kiapo cha kulinda na kuhifadhi siri ya kundi na kuwa tayari kufa kuliko kutoa siri ya kikundi. Vilevile kuwa tayari kuuawa pale nitapobainika nimetoa siri.

Baada ya kiapo ndipo nilipotambulishwa kwa wajumbe wa kikao kile,  wageni kulikuwa na raia wa Pakistan, Columbia, Afrika magharibi , Uturuki, Marekani ya kusini.

Baada ya kutambushwa kwao Father Gin alinigeukia mimi:

“Ndugu wajumbe wa mkutano wa PT au Pigo Takatifu huyu ndiye tuliyemwandaa kwa ajili ya Operesheni  Pigo Takatifu. Leo hii kama tulivyoongea kwenye kikao chetu jukumu lote tunamkabidhi binti ambaye nina imani ataifanya kazi vizuri na kuweza kufanikisha opereshemi yetu, Thereza,” aliiniita:

“Abee.”

“Nina imani lazima utashangaa na kujiuliza ni kazi gani hiyo yenye malipo mazito lazima utakuwa na wasiwasi. Kweli kazi ni nzito inabidi mafunzo ya kina ndio maana tulikuandaa kwa ajili ya kukabiliana na kazi nzito. Malipo tuliyotoa ni kulingana na kazi nzito ambayo maisha ya muhusika huwa hatarini kwa asilimia tisini, ndio maana tumetoa malipo manono pindi mtu wetu akifariki kazini kwa ajili ya watu wanaomtegemea.

"Leo hii utakabidhiwa pesa zako taslimu bilioni 60 na umalizapo kazi yetu tutakupatia bilioni 40 zilizobaki kama utaifanikisha lazima tutakupa zawadi, mimi kama mimi ninakuahidi bilioni 30 sijui wenzangu,” aliwageukia wenzake.

“Sisi hatuahidi ila ataona baada ya kazi,” walijibu wajumbe wa mkutano.

“Kwanza kabla ya kukueleza ni kazi gani lazima uelewe sababu za kukupa hiyo kazi. Hili unaloliona ni kundi la watu kumi na sita hapa tupo watu kumi na mbili na wanne  waliojitoa.

"Kundi hili lina shughuli nyingi ambazo ni siri zisizojulikana na mtu yoyote zaidi yetu sisi kumi na sita. Kwanza kabisa mimi ndiye muasisi wa kundi hili nchini na kuanza kukusanya watu walio tayari kufanya kazi nami nashukuru niliwapata na wakanielewa.

"Kundi hili lina sura mbili, kwa nje lina sifa nzuri kwani lipo mbele kutoa msaada kwa jamii ambao hudhani wanakula kumbe wanaliwa. Msaada tunaoutoa kama

kujenga makanisa makubwa bila msaada wa sadaka, huduma vijijini kama maji,umeme hospitali na huduma nyingine kwa jamii.

“Kitu kinachofanya watu wajenge imani juu yetu. mradi wa makanisa au kujenga vituo vya msaada ili kuwavuta karibu na kufanikisha azma yangu. Mradi tulioanza nao ni wa kuuza damu, nina imani kazi hiyo hata wewe uliifanya bila kujua. Ulipompata mteja na kumuacha hotelini vijana wetu aliingia na kumnyonya damu na kumchuna ngozi yake.

"Biashara hii  inatuingizia pesa nyingi sana hasa baada ya wakubwa wengi kuathirika na ugonjwa wa ukimwi. Katika watu walioliingizia faida kubwa ulikuwa wewe hivyo tulikuandaalia asante lakini ajabu ulipotea kiajabu.

"Mradi wetu wa uuzaji wa damu nchi za nje uliingia dosari baada ya kugundua damu nyingi za watu wazima zimeathirika hivyo ndivyo tulivyobuni njia nyingine ya kupata damu iliyo safi kwa kuanzisha mradi wa kukusanya vijana kwa njia ya kuwapeleka nje kusoma au kufanya kazi.

"Kutokana na jinsi tulivyojijenga wazazi wao hawakuwa na pingamizi njia ile ilitusaidia  kupata damu iliyo safi na biashara ya ngozi za watu. Ndani ya miaka mitano tulitengeneza pesa nyingi sana. Hakukuwa na biashara hiyo tu vilevile tulitumia kivuli cha kanisa kuingizia dawa za kulevya pamoja na kusafirisha madini na nyara za serikali nje.

"Ukweli kivuli cha dini kilituingizia pesa nyingi mpaka leo hii ni nani atayeamini kuwa sisi tunahusika na kazi hii hata mheshimiwa Rais sijui kitu zaidi ya kutupa ushirikiano na yeyote aliyetaka kufuatilia nyendo zetu tulimpoteza.

"Muungano wetu uliingia ufa miaka miwili iliyopita ufa  baada ya wenzetu wanne kujitoa ambao waliweka mpasuko mkubwa. Mpasuko huo ulisababisha hata biashara yetu ya damu na ngozi za watu zikose soko na kusababisha tupate hasara ya trion 20.

“Vilevile kupotea mkataba wa trilioni 150 ambazo ni malipo yetu ya uuzwaji wa damu, ngozi, pembe na madini tuliyo wapelikea mawakala wetu.

"Hizo zilikuwa njama za wenzetu manne waliojitoa hasa Marry White ambaye ni mpenzi wa bosi wa shirika tuliokuwa tunawapelekea vitu vyetu. Cha kushangaza disc iliyokuwa na mkataba wa malipo ilipotea katika mazingira ya kutatanisha hata kumbukumbu nazo zilikuwa  zimefutwa kwenye Computa.

"Tuliogopa kuwajulisha tumepoteza disc hata kumbukumbu, Mary White na wenzake wana mpango wa kuchukua zile hela ambazo ni nyingi sana. Kama watazichukua litakuwa pigo kubwa kwetu.  

"Cha kufanya ni kuhakikisha watu hawa wanauwawa vilevile utumie ujuzi wako uweze kupata mkataba huu ambao upo katika ofisi za mawakala wetu. Utafanyaje? Sisi hatujui ndio maana tumekupa mafunzo mazito tofauti. Watu hawa ni hatari mafunzo yao na wewe hayatofautiani sana ila yako yamezidi.

"Ila wao ni wazoefu na kazi za mauaji ni watu makini sana hawana mchezo hasa Marry White ni mwanamke hatari sana hasa akigundua wewe ni adui yake anaweza kukufuata huku huku na kukumaliza..

 "Mwanzo tuliwatumia vijana wetu wenye uwezo mdogo walikufa kama nzige, wengine walikufa hapahapa siku tuliyopanga waondoke ndio siku waliouawa kinyama.

 Kitu kilichotutisha na kujua vita hii ni nzito ambayo inahitaji kujipanga  vizuri.

Uamuzi tuliouchukua ndio wa kukuandaa wewe ili ukabiliane na tatizo lililo mbele yetu tuna imani kubwa na wewe kuwa utaiweza.”

Muda wote aliokuwa akiongea Father Gin  macho yake yalikuwa hayachezi mbali na paji la uso wangu, nami vilevile sikuchezesha macho yangu zaidi ya kumwangalia na kumsikiliza kwa makini habari ambazo zilinisisimua.

Sio siri habari zile zilifanya nimkumbuke mzee wangu mtu niliye muona ana umuhimu wa pekee mzee Utakufalini. Maelezo yao yalikuwa sawasawa na aliyonieleza juu ya kugundua unyonyaji wa damu na uchunaji wa ngozi za binadamu. Hapo ndipo nilipogundua muuaji harisi wa familia ya mzee Utakufalini ni Father Gin. 

Akili yangu uligundua kitu kingine na kuona kumbe duniani wapo watu wanaotumia vivuli vya ukarimu ili kuficha maovu yao, tena wanatumia vivuli vya udini au taasisi ili kuifumba macho serikali na wananchi wake.

 "Thereza," nilishtushwa na sauti nzito ya Father Gin.

"A..bee," nilikuwa kama natoka ndotoni.

"Naona upo mbali vipi umenielewa?”

"Ni kweli"...maana kazi iliyopo mbele ni sawa na kuchezea ndani ya kinywa cha mauti."

“Usemayo ni kweli ndio maana tumekupa mafunzo ya kutosha ili kukabiliana nayo vilevile tumetoa malipo manono kwa kuzingatia uzito wa kazi.”

“Sasa ni hivi.." Father Gin alinyamaza kidogo na kupiga funda mbili za Whisky kisha aliendelea kusema:

"Thereza, nilikuwa sijamaliza maelezo yangu."

 "Endelea tu Father."

 "Mpasuko uliotokea kwenye kikundi chetu umesababisha shughuli zetu zote zisimame hata uvunaji wa vijana nao ulisimama ilibidi tutafute sehemu tuwahifadhi hao vijana ili kusubiri hali ikitulia tuweze kuvuna damu na ngozi na hakuna njia nyingine ni kuwaua hawa watu wanne Marry White na wenzake ambao wote wapo Italy na England.

“Ukifanikiwa kuwaua hawa utakuwa na kazi nyingine ya kwenda Ujerumani ambapo ndipo makuu ya wakala wetu mnunuzi mkuu wa vitu vyote tunavyo vivuna hapa nchini na nchi zingine za Afrika.

“Matawi yetu yapo Kenya, Uganda, Sudan, Afrika ya kusini, Nigeria na Senegal. Sehemu zote hizi tuna wakala wetu wanaokusanya watoto wa kivuli cha kituo cha kulelea watoto wenye maisha magumu. Ukweli mradi huu umetuingizia pesa nyingi sana, mradi wenye siri kubwa iliyojificha nyuma ya pazia. Na sio kwamba hakuna mawakala wengine ila tunaogopa tukibadili wakala hapo lazima tutapoteza pesa zetu trilion 150.

Sijui una swali lolote juu ya yote niliyokuileza?" Father Gin aliniuliza.

Kabla ya kuuliza swali nilikohoa kidogo kisha niliuliza.

"Samahani Father Gin."

"Bila samahani."

"Unataka kunieleza kuwa kuna baadhi ya watu waliouawa ndani na nje ya nchi pale wanapotaka kufuatilia jambo hili kati ya hao kuna mtu aliyepata mwanga wowote?"

"Hakuna."

"Hao ulio watuma wana ujuzi gani?"

 "Ujuzi wao si mkubwa sana ila ni wazoefu.”

"Huoni kama uliwauza?" nilimuuliza swali.

"Kuwauza kivipi?”

"Utampelikaje  mtu akapambane na mtu aliyemzidi uwezo?”

‘”Tulifanya kama shambulizi la kushtukiza.”

“Kama shambulizi la kushtukiza iweje wafe kirahisi namna ile?”

“Kwa kweli hata sisi ilitushitua.”

"Usinichekeshe Father Gin iliwashtua kivipi ikiwa bado mliendelea kuwatumia vijana wasio na ujuzi, mbaya zaidi unasema waliuawa hapahapa nyumbani kabla hawajaondoka huoni vita ipo hapahapa wala sio huko mnapotutuma?”

“Maneno yako ni mazito uliyosema sio kwamba tulikuwa na nia mbaya na wote walio uawa, ukweli tulichanganyikiwa tusijue nini cha kufanya," Father Gin alijitetea baada ya kumbana.

 "Si kweli siwezi kukubaliana na usemacho yaani watu wanne wawazidi akili watu kumi na mbili tena inafikia hatua watu wanaingia mpaka ndani, nauliza adui yupo wapi ili nikianza kumtafuta nijue na mtafutia wapi?"

"Swali lako ni gumu."

“Kama unaelewa au huna habari ndani ya kikao hiki kuna watu wanatoa siri za kikao hivyo hakuna kitu kitachofanyika. Hata nikikubali nitakuwa nimesaini kifo, nitawezaje 

kupigana na mtu nisiyemjua, naye ananijua vizuri mbaya yeye

yupo gizani mimi nipo peupe naonekana. Hamuoni hapo nakichezea kifo, ni wazi adui yenu anawaeleweni vizuri, kuliko ninyi mnavyo muelewa yeye. 

“Nikinukuu kauli yako kuwa  Marry White anatisha yupo tayari kumfuata 

adui yakepopote alipo  pale atapojua unamtafuta ni wazi anajua kuwa

mimi nimeandaliwa kwa ajili yao lazima watanizima kabla sijaianza 

kazi yenyewe.

“Kwa nini hakunieleza mapema wala nisingekubali kupoteza muda wangu kwenye 

mafunzo, nitawezaje kushindana na mtu anaye nifahamu. Inasikitisha mtandao mzito kama huu siri zenu zivuje. Lazima mchunguzane wenyewe kwa hali hii sipo tayari kuifanya kazi hii vilevile nipo tayari kuwalipeni gharama zenu zote."

"Usifike huko Thereza wewe ndiye tegemeo pekee la kundi letu tutakulinda."

"Usinichekeshe, mmeshindwa vipi hao mniweze mimi kwa taarifa yenu sitasaini mkataba vilevile nawahakikishieni siri hii itabakia moyoni mwangu mpaka naingia kaburini ila onyo mtu yoyote asinifuatilie nyendo zangu tutaonana wabaya,"  mtoto wa kike nilitoa mkwara mzito.

"Thereza usifanye hivyo basi sema unataka kiasi gani zaidi ya Bilioni 100 sema tupo tayari kukupa."

“Father Gin nielewe, ukitaka tuongelee habari ya kazi uondoe unafiki ndani ya kundi lako hapo tutakuwa tayari kuifanya kazi yako."

"S...sa....asa..."

"Hakuna cha sasa fanyia kazi niliyo kueleza kwa heri."

Nilinyanyuka na kuondoka bila kugeuka nyuma. Wote walibakia midomo wazi, nilitoka hadi ofisini kwa Dk Ray.


ITAENDELEA...


Post a Comment

0Comments

Your Thoughts

Post a Comment (0)